Friday, January 05, 2018

PAUL MAKONDA AMEWAWEZESHA WANYONGE KUTIBIWA BURE

                             PAUL MAKONDA AMEWAWEZESHA WANYONGE KUTIBIWA BURE
Mkuu wa Mkoa wa Dar e s Salaam Paul Makonda amekuwa akifanya jitihada kubwa za kuwapunguzia gharama za matibabu wananchi wenye kipato cha kawaida(wanyonge) Ni hivi karibuni wagonjwa wasiopungua 10,000 waliweza kupata matibabu bure. Meli iliyokuwa na madaktari bingwa kutoka nchini China ilitoa huduma hiyo kwenye bandari ya Dar es Salaam. Wananchi wengi waliojitokeza waliweza kupimwa na kutibiwa magonjwa mbalimbali. Magonjwa hayo ni kama vile shinikizo la damu,Kisukari,Saratani  na mengine ambayo wananchi wa kawaida wasingeweza kutibiwa kwana gharama za matibabu ni kubwa.
Lakini hata kabla ya madaktari hao wa kichina kuja kutoa huduma za matibabu, mkuu huyo wa mkoa alikuwa tayari amefanya ushawishi kwa madaktari hapa nchini kuwapima na kuwatibu wagonjwa. Watu wengi wamekuwa wakijitokeza kupokea huduma hiyo, ingawaje idadi ya wahitaji bado ni kubwa. Kiongozi huyo amekuwa akiwahimiza watanzania kujenga utamaduni wa kupima afya zao, kwani ni muhimu kwao kufahamu hali za afya zao ili kuweza kukabiliana na magonjwa ya hatari.
Makonda anaamini kuwa ikiwa kila mwananchi atakuwa na afya njema, ni dhahiri atakuwa na uwezo wa kutoa mchango mkubwa katika ujenzi wa taifa lake. Kitu kingine ambacho Makonda ameweza kuwathibitishia wananchi katika ubunifu huo, ni uwezo wake wa kuonesha serikali inaweza kuwatibu bila kulipia fedha.
Enzi ya watanzania kutibiwa bure ilikoma wakati wa utawala wa awamu ya kwanza ya hayati Baba wa Taifa,Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Kujitokeza kwa wingi kwa wananchi wanaohitaji matibabu ya bure, ni kiashiria kwa serikali kutambua kwamba wananchi wanapenda kupimwa afya na kutibiwa, lakini gharama ziko juu.
Ubunifu wa Makonda wa kupima na kutoa matibabu bure kwa wananchi, umekuwa ukiwalenga zaidi wakazi wa mkoa wa Dar es Salaam. Hata hivyo wahitaji, wahitaji ni wengi na wakazi wa mikoa mingine wamekuwa wakijitokeza. Kwa siku zilizopita, Rais wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli alimsifu Makonda kwa ubunifu ambao amekuwa akiufanya na kuijengea heshima serikali yake. Alitoa mwito kwa wakuu wa mikoa mingine hapa Tanzania kuiga kile kilichokuwa kikifanywa na kiongozi huyo. Na ndiyo maana  basi kwamba kama wakuu wengine wa mikoa wangewahamasisha madaktari kwenye mikoa yao, watu wengi zaidi wangenufaika na vipimo na matibabu ya bure.
Makonda alipokuwa mkuu wa wilaya ya Kinondoni aliwahamasisha wamiliki wa magari ya abiria jijini Dar es Salaam (Daladala) kuwasafirisha waalimu wote bure wakati wanapokwenda na kurudi kutoka kazini. Alifanya hivyo kwa kutambua hali ngumu ya maisha inayowakabili waalimu wa mkoa wa Dar es Salaam na  Tanzania kwa ujumla.
Makonda hali kadhalika anaendelea na jitihada za kuhamasisha watu mbalimbali wasaidie mradi wa kujenga ofisi za walimu. Amepata mwitikio ndani na nje ya nchi. Ubalozi wa China hapa nchini umetoa fedha nyingi za kumuunga mkono Makonda ili afanikishe ujenzi wa ofisi za walimu mkoani Dar es Salaam.
Ubunifu wa Makonda unajitofautisha na wakuu wa mikoa wenzake. Badala ya kuamrisha taasisi,mashirika ama wananchi wafanye nini, yeye ubunifu wake umekuwa ukilenga kuhamashisha na kisha kutanzua tatizo analoliona kwa jamii. Kwa mfano, wananchi waliobahatika kupimwa na kutibiwa bure watamkumbuka Makonda kuwa kiongozi anayetetea ustawi wa maisha yao kwa kuyapigania. Wakiisha kuwa na afya njema,nao watakuwa tayari kulitumika taifa kwa moyo wote na kuliwezesha kupata nguvu ya kiuchumi katikati ya mataifa mengine duniani. Makonda anastahili kupongezwa kwa kutetea afya za watanzania ambao kwao ni mtaji mkubwa.