Monday, January 08, 2018

RUSHWA INAWEZA KUTOKOMEZWA,TUZIDISHE MAPAMBANO


 Image result for picha ya raisi magufuli
Shirika lisilo la kiserikali la Twaweza lilitoa taarifa ya hali ya rushwa hapa nchini.Mkurugenzi Mtendaji wa Twaweza Aidan Eyakuze alieleza kuwa viwango vya rushwa vimepungua kwa mwaka 2017 ukilinganisha na mwaka 2014.Hata hivyo taasisi mbili za serikali zilikuwa bado zinaongoza kwa vitendo vya rushwa.Taasisi hizo ni Jeshi la Polisi na Mahakama. Kwa mfano kwa mwaka 2014, vitendo vya rushwa vilifikia asilimia 60 lakini vikashuka kwa asilimia 39 kwa mwaka 2017.

Ingawaje tatizo la rushwa haliwezi kuisha kabisa,  walio wengi waliyapokea matokeo ya utafiti huo ulioonesha  kupungua kuwa ni kiashiria kizuri cha ushindi wa mapambano dhidi ya rushwa. Zipo jitihada zilizofanywa na serikali ya awamu ya tano katika kudhibiti kuenea kwa rushwa na matumizi mabaya ya madaraka. Kuna kesi zilizofunguliwa mahakamani.Baadhi ya watuhumiwa wamehukumiwa na kutumikia vifungo gerezani. Wanaoendelea kupokea ama rushwa bila shaka wanajua kikamilifu kuwa siku zao zinahesabiwa.

Pamoja na utafiti huo kubainisha rushwa kupungua, kulikuwa na mawazo ya watu waliohojiwa wakieleza mapambano dhidi ya rushwa yanadidimiza kukua kwa uchumi.Mawazo kama hayo yalikuwa ni ya kushitua ndani ya fikra za watu wanaopambana na vitendo vya rushwa. Ilikuwa ni tafsiri ambayo haina maelezo ya kuridhisha kwani uchumi unaathirika vipi katika mapambano hayo wakati wananchi wanaporwa haki zao? Je, mawazo ya namna hiyo yanawakilishwa na kundi gani? Ni kundi la walionacho ama wasionacho? Ni dhahiri hayo yalikuwa ni mawazo ya walionacho..

Kwa mfano uchumi unaathirika vipi ikiwa wananchi wamekuwa wakilazimishwa na watumishi wa serikali kulipia huduma ambazo wangezipata bure? Kwa utawala wa awamu ya tano ambapo wananchi wanasifia huduma zimeimarika, Je, si ndiyo uchumi unaimarika zaidi kwani imani yao kwa serikali imeongezeka. Miaka michache iliyopita, wananchi walikuwa wamepoteza imani kwa serikali yao jambo ambalo lilikuwa ni hatari kwa sifa na uchumi wa  taifa letu.

Ilikuwa imefikia hatua ambapo wananchi wa kawaida walikuwa wanajiona kuwa wao si chochote wala lolote mbele ya watumishi wa umma. Nao watumishi wa umma wakawa wanajiona kuwa mabwana wa kuwafanyia watakavyo wananchi wa kawaida.Tunaisikia kauli mbiu ya Rais Dk. John Pombe Magufuli akiweka waziwazi kuwa serikali yake itawatumikia wanyonge. Kauli hiyo inatolewa na kiongozi huyo kwa kufahamu kile kilichokuwa kikiwapata wananchi wa kawaida walipokuwa wakitaka huduma kutoka kwa watumishi wa umma.

Mojawapo kati ya maamuzi ambayo yanakubaliana na kauli hiyo ni kuwaruhusu wachimbaji wadogowadogo wa madini kufanya shughuli zao bila kubughudhiwa. Ukiutafakari uamuzi huo, unaweza kugundua kuwa kulikuwa na viashiria vya rushwa vilivyokuwa vikiwapendelea wachimbaji wa madini wa makampuni makubwa.Kufuatia hali hiyo, tulikuwa tukisikia jinsi wachimbaji wa madini wadogowadogo walivyokuwa wakipigwa  virungu na Polisi,kuumizwa na hata kuuawa wakiwatetea wachimbaji wa makampuni makubwa. Wao ndiyo  walikuwa na haki zaidi ya watanzania wazalendo.

Na uamuzi huo ni dhahiri kwamba Dk. Magufuli anaamini endapo wachimbaji hao wanaporuhusiwa wataisaidia serikali katika kulipa kodi na hivyo kuongeza pato la serikali.


Dk. John Pombe Magufuli  alikuwa hajaridhishwa na jinsi Kampuni kubwa za kuchimba madini zilivyokuwa zinalipa kodi. Hilo liliweza kuthibitishwa pale makontena ya mchanga wenye dhahabu yalipokamatwa kwenye bandari ya Dar es Salaam.Kampuni ya Barrick Gold Corporation ilipojitokeza kukiri kuwa mmiliki wa makontena hayo, ilibainika ilikuwa ikikwepa kulipa mamilioni ya kodi. Kwa namna yoyote hatuwezi kukana ukweli kwamba huo ulikuwa ni  mmojawapo wa  mikakati wa kupambana na vitendo vya rushwa. Tumesikia kuwa baada ya kukiri kukwepa kulipa kodi hiyo, sasa Kampuni ya Barrick Gold Corporation imekubali kuilipa serikali ya Tanzania kiasi cha shilingi bilioni 700. Ni dhahiri fedha hizo zitasaidia katika kuwaletea wananchi maendeleo yanayotakiwa. Kama serikali isingesimama imara, fedha hizo zingewanufaisha watu wa mataifa ya nje na kuwaacha watanzania katika umaskini.Watanzania wote kwa ujumla wanapaswa kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya rushwa. Ikiwezekana rushwa itokomezwe kabisa.