WASAFIRI WA MWEZI
DESEMBA WATAFARIJIWA NA KUKAMILIKA KWA TRENI
YA KISASA

Kila unapofika mwezi Desemba kila mwaka,watu wengi
hushawishika kusafiri kuliko miezi mingine yoyote.Sikukuu za Krismas na mwaka mpya,
zinatoa msukumo kwa watu kusafiri kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine. Wengi
hupendelea sikukuu hizo ziwakute ama
ziwaunganishe na familia zao. Katika hali ya kawaida, mwezi wa Desemba
umekuwa na ongezeko la ajali nyingi za
barabarani. Magari huwa yanabeba abiria wengi kupita kiasi na wakati huohuo
madereva wa magari ya abiria kuzembea kuzingatia kanuni za usalama barabarani.
Askari wa usalama barabarani wanakuwa na kazi kubwa ya kukagua na kuhakikisha
madereva wa magari ya abiria wanaendesha kwa makini ili kuepusha ajali.
Ni katika kipindi cha mwezi huu wa Desemba, ambapo nauli za
mabasi ya abiria huongezeka maradufu.
Baadhi ya wamiliki wa mabasi ya abiria hukitumia kipindi cha mwezi wa Desemba,
kujitafutia faida kubwa kwani wanafahamu watu wengi wanapenda kusafiri. Ni
katika mwezi huu wa Desemba vitendo vya udanganyifu na utapeli huwa vinaibuka
na kuwasababishia hasara abiria.
Kusafiri kila unapofika mwezi Desemba ni vizuri, kwani siyo
hapa Tanzania
tu bali hata huko Ulaya idadi ya
wasafiri huongezeka. Tofauti inayojitokeza huku kwetu, ni uchache wa mabasi ya
abiria yanayotosheleza mahitaji yao .
Kwa kadri ya safari za mwezi Desemba abiria wengi wamekuwa wakilazimika kulala
kwenye vituo vya mabasi, wengine kujazana na kukosa viti vya kukalia na kugeuka
kuwa kero na taabu kwao.
Katika kukabiliana na ongezeko kubwa la wasafiri kwa mwezi
Desemba, wakati uliopita serikali ilikuwa ikilazimika kutoa vibali kwa taasisi
ama Kampuni nyingine kusafirisha abiria. Ninakumbuka Chuo cha Usafirishaji cha
Taifa (NIT) kiliwahi kushiriki kusafirisha abiria katika msimu wa mwezi
Desemba. Hata kwa sasa kama serikali inaweza kutoa maamuzi kama
hayo mapema, itasaidia kuwapa faraja wasafiri kuondokana na kero zinazojitokeza
mwezi Desemba.
Lakini lililo bora zaidi katika kuleta faraja kwa
watanzania, ni pale ujenzi wa reli ya kati ya kisasa kutoka Dar es Salaam
kuelekea Kigoma na Mwanza, na ile inayoelekea mikoa ya Kaskazini itakapokuwa
imekamilika. Abiria wataweza kusafiri kwa Gari Moshi Unafuu wake unatokana na
ukweli kwamba nauli zake zitakuwa nafuu ukilinganisha na nauli zinazotozwa na
mabasi ya abiria.
Usafiri kwa Gari Moshi ni salama zaidi. Hakuna tishio la
kuvamiwa na majambazi kama ilivyo kwa usafiri
wa magari ya abiria ambao huvizia kutafuta fedha.Usafiri kwa Gari Moshi
utaisaidia serikali kuokoa maisha ya watanzania wengi wanaofariki kutokana na
ajali zinazotokea mara nyingi mwezi wa
Desemba.
Kwa sasa hivi ni kama vile
abiria wenye vipato vya kawaida, wanalazimika kusafiri kwa mabasi.Lakini pale
reli hizo zitakapokuwa zimekamilika zitawawezesha abiria kupanga na kuchagua
aina ya usafiri wanaoupenda. Ni ukweli unaokubalika kwamba wengi wanapenda
kusafiri mwezi Desemba kwa sababu
zilizojadiliwa kwenye makala hii,wakati mwingine inakuwa ni kero kubwa
kwa kufikiria matatizo ya usafiri yakiwemo ajali ama wizi.Serikali kwa dhamira
yake ya kujenga reli ya kisasa, iharakishe kuikamilisha na itakuwa neema kwa
watanzania watakaokuwa wakisafiri kila unapofika mwezi Desemba.Watakuwa na
fursa ya kupanga bila hofu safari zao.