Monday, November 20, 2017

AMANI YA TANZANIA ISICHEZEWE NA WAFUGAJI KUTOKA NCHI MAJIRANI

Related image

Serikali ya Tanzania imeamua kwa dhati kabisa kupiga mnada maelfu ya ng’ombe wote
wanaoingizwa nchini kinyume cha sheria kutoka kwa nchi majirani.Nchi majirani wa Tanzania ambao ng’ombe wao wamekuwa wakiingizwa nchini kwa kisingizio cha kutafuta malisho ni Kenya, Uganda na Rwanda.
 
  Alipokuwa kwenye ziara ya kikazi mkoani Kagera,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli alisisitiza msimamo huo. Magufuli anasema kwa kuwa Tanzania inafanya hivyo, vivyo hivyo na nchi majirani wa Tanzania wawapige mnada ng’ombe watakaokuwa wameingizwa kinyume cha sheria kutoka nchini Tanzania.
  Licha ya Kenya,Uganda na Rwanda kuwa majirani, lakini pia ni wanachama wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki. Matamshi ya Rais Dk. John Pombe Magufuli kuhusiana na uingizwaji wa mifugo, yaliwashitua baadhi ya watu.lngawaje tayari kiasi cha ng’ombe zaidi ya 1000 kutoka nchini Kenya walikuwa wamepigwa mnada.Yalikuwepo malalamiko kutoka kwa waliodai kuwa walikuwa wamiliki wa ng’ombe kutoka nchini Kenya, lakini serikali ilisema waliopigwa mnada hawakuwa na mmiliki wake.

Katika mahusiano ya ujirani mwema, kulikuwa na matumaini kwamba serikali ya Tanzania ingeweza kuwaonea huruma wafugaji wanaoingiza  nchini ng’ombe wao kinyume cha sheria. Kulikuwa na madai kwamba serikali ya Tanzania imefanya makosa makubwa kiasi cha kuhatarisha ushirikiano wa mataifa hayo ya Afrika ya Mashariki.Msimamo wa serikali ya Tanzania unazidi kusisitiza kwamba hakuna ushirikiano katika uhalifu. Kwa maana hiyo wafugaji kutoka nchi majirani wanaoingiza mifugo yao kinyume cha sheria wanapaswa kushughulikiwa kama wahalifu wengine.

Tanzania inayo ardhi kubwa. Inatoa ushawishi kwa nchi majirani kudhani kwamba wafugaji wanaweza kuvuka mipaka na kufanya watakavyo kwa kisingizio cha ushirikiano uliopo miongoni mwa mataifa hayo,kumbe sivyo.Tanzania inastahili kuzionya nchi majirani kwa kutoa adhabu kali dhidi ya wafugaji wakorofi. Hapa hapa nchini tatizo la wingi wa mifugo bado ni tatizo linalosababisha athari mbalimbali miongoni mwa wakulima na Wafugaji. Kumekuwa na matukio ya wafugaji na wakulima kupigana, kujeruhiana hadi kuuana. Maisha mengi ya watanzania yamekuwa yakipotea kutokana na wingi wa mifugo.

Mwanzoni ilidhaniwa serikali ya Tanzania inakabiliana na tatizo la mifugo ya  watanzania, kumbe ndani yake wamo wafugaji kutoka nchi za Rwanda,Uganda na Kenya.Fikiria ni mzigo kiasi gani unaobebwa na  serikali ya Tanzania kwenye suala hilo? Ni haki kweli serikali inyamaze eti kwa kuhofia kuvuruga uhusiano na majirani zake? Siyo hivyo tu, baadhi ya watanzania walikuwa wanafanya biashara ya kutunza mifugo ya wafugaji kutoka nchi majirani.

Yako matumaini makubwa kwamba baada ya serikali ya Tanzania kutoa msimamo huo kwa kutoa adhabu kali, migogoro ya muda mrefu ambayo imekuwa ikiwanyima amani watanzania kuhusiana na mifugo itakuwa imepata ufumbuzi.Mwanzoni ilidhaniwa ni tatizo la ndani kumbe hata majirani zetu wamekuwa wakichangia katika kuleta matatizo ya majeruhi  na maafa. Amani na utulivu hapa nchini iliyodumishwa kwa muda mrefu na viongozi waliopigania uhuru, ilikuwa ikiharibiwa kwa ushirika wa nchi majirani.
Kama ambavyo serikali imekuwa haina huruma dhidi ya watu, kikundi ama taasisi kinachokusudia kuvuruga amani ya watanzania ni wakati sahihi kutofanya mzaha wa kuchezewa na wafugaji kutoka mataifa ya nje.

Wafugaji wanaoingiza mifugo kinyume cha sheria kutoka nchi jirani, wanapaswa waadhibiwe kikamilifu kwa kujulishwa wanachokifanya ni sawa na kuchezea amani, usalama na utulivu hapa nchini.Imekuwa siyo siri kwamba katika uingizwaji wa mifugo, makundi ya uhalifu mbalimbali yamekuwa yakijificha kama vile majangili hata majambazi.

  Sekta ya Utalii imekuwa ikiathirika kutokana na wanyama wanaowashawishi watalii kuja nchini kupungua ama kutoweka kabisa. Zipo taarifa za kupungua kwa idadi ya Tembo na hata wanyama wengine. Ni bora kabisa kwa serikali ya Tanzania kudhibiti na kukomesha kwa kutoa adhabu kali wafugaji kutoka nchi za majirani kwa faida ya amani na utulivu wa taifa letu.