Monday, November 20, 2017

HISTORIA ISIMSAHAU ROBERT MUGABE HATA AKING’ATUKA ZIMBABWE

Image result for mugabe zimbabweWazimbabwe na wananchi wa mataifa mengine wanayo shauku kubwa kusikia Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe anang’atuka kwa kupenda ama kwa lazima. Rais Robert Mugabe amekuwa kiongozi wa Taifa hilo tangu mwaka 1980,nchi hiyo ilipojipatia uhuru kutoka kwa wakoloni wa Kiingereza. Kwa sasa anao umri wa miaka 93. Wanaomtaka Robert Mugabe ang’atuke, wanasema amekuwa madarakani kwa muda mrefu. Yeye mwenyewe mpaka sasa anasema anataka awe madarakani hadi hapo uchaguzi utakapofanyika. Kwa siku zilizopita aliwahi kusema yeye atakuwa Rais wa Maisha. Siyo muda mrefu kutoka sasa, kiongozi mmoja wa dini alifikia hatua ya kutabiri kwamba Rais Mugabe angefariki mwaka huu.

Jeshi la Ulinzi la Zimbabwe wiki hii lilitangaza kutwaa utawala wa taifa hilo, lakini lilikana kufanya mapinduzi ya kumuondoa madarakani Rais Robert Mugabe. Rais Mugabe alizuiliwa asitoke nyumbani kwake, lakini jana (Ijumaa) aliweza kuhudhuria sherehe za mahafali ya chuo kikuu huria mjini Harare na kutunuku shahada kwa wahitimu mbalimbali.

Kumekuwa na majadiliano kati yake na wanajeshi wanaoongozwa na mkuu wa Jeshi la Zimbabwe Costantine Chiwenga,wakishinikiza Mugabe atangaze kustaafu  u rais wa nchi hiyo na kumuachia Makamu wake,Emmerson ‘Mamba Mnangagwa anayekubalika kwa wanachama wa Chama tawala cha ZANU-PF na wanajeshi. Na wakati huo huo, viongozi wa mataifa ya nchi za Jumuiya ya maendeleo kwa nchi za  kusini mwa Afrika(SADC) nao wanakutana kujadili namna ya kupata suluhisho la mgogoro ulioko huko Zimbabwe.

Hata hivyo msimamo wa viongozi wa SADC ni kuhakikisha kwamba mgogoro huo unatanzuliwa kwa kuzingatia katiba ya nchi hiyo. Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika Alpha Conde naye hali kadhalika aliungana na msimamo wa viongozi wa SADC. Alikilaani vikali kitendo kilichofanywa na Jeshi la Zimbabwe na kusema kamwe hakitambui wala kuunga mkono.

Viongozi wa mataifa ya Ulaya kama vile Uingereza, Ujerumani ama Marekani ambayo kwa wakati uliopita yalikuwa yakimtaja Robert Mugabe kama kiongozi ‘dikteta’, yameutaka mgogoro huo umalizwe kwa majadiliano na kwa kufuata katiba ya nchi.
Robert Mugabe uhusiano wake na mataifa ya Ulaya ulitetereka kutokana sera yake aliyoifanya ya kutaifisha mashamba yaliyokuwa yakimilikiwa na wazungu na kisha kuwagawia wazimbabwe.

Kulikuwepo na ukosoaji mwingi uliokuwa ukipinga maamuzi mazito ya Robert Mugabe kwamba yalikuwa ndiyo sababu ya kuporomoka kwa uchumi wa taifa hilo.Bei za vyakula na bidhaa mbalimbali zimekuwa zikiuzwa kwa bei ya juu, na inasemekana maisha ya wazimbabwe yamekuwa ni magumu.

Kiongozi wa chama cha upinzani, Morgan Tsavangirai aliyewahi kushindana na Mugabe katika medani za siasa, hakuweza kufaulu kumuondoa madarakani Rais Robert Mugabe.Kulikuwa na madai kwamba Morgan Tsavangirai alikuwa ni kibaraka cha mataifa ya nchi za ulaya ya Magharibi. Katika mojawapo ya hotuba zake kwa wale waliokuwa wakimtaka aondoke madarakani, Robert Mugabe alikuwa akisema kwamba asingeweza kukubali kumwachia nchi yake ya Zimbabwe ‘ kibaraka’ ambaye hajui mateso ya wakombozi wa Zimbabwe walipokuwa wakipigana vita msituni.Inawezekana kitu kinachompa mashaka kiongozi huyo ni mapenzi yake ya dhati dhidi ya nchi yake. Anajiuliza, je, haitatokea kwa kiongozi atakayechukua nafasi yake kuirejesha tena kwa wakoloni? Maswali hayo yanamnyima raha

Inawezekana kabisa kwamba wazimbabwe walikuwa wamemvumilia Robert Mugabe, lakini maamuzi yake ya kutaka kumrithisha mke wake Grace, ndiyo yanayozidisha chuki ya wazimbabwe dhidi yake. Na hilo ni kosa kubwa na baya kabisa kwa kiongozi kuifanya familia yake kuendelea kutawala kana kwamba inatawaliwa kifalme.Wanaopinga utawala wa Robert Mugabe wanasema taifa hilo sasa lilikuwa linaongozwa na mke wake Grace kiasi kwamba hata hotuba zake alikuwa hawezi kuziandaa.

Ni katika hali ile ile kwamba viongozi na wanachama wa ZANU-PF hawakubaliani Grace ampokonye cheo aliyekuwa makamu wa Rais,Emerson ‘Mamba’ Mnangagwa. Grace hakubaliki kwa kuwa hakutoka jasho la kuikomboa Zimbabwe kutoka kwa wakoloni kama ilivyo kwa Mnangagwa.

Ingawaje walio wengi wanamtaka Robert Mugabe aondoke madarakani, lakini atakumbukwa kwa msimamo wake usiolegalega hususan kwa mataifa ya Ulaya.Aliweza kuthubutu kuyaambia bila woga yaache kuingilia masuala ya waafrika. Mpaka sasa Rais Mugabe ni miongoni mwa viongozi wa serikali ya Zimbabwe waliozuiliwa kuingia katika nchi za Ulaya.

Mwananchi mmoja akiwa nchini Zimbabwe na kuhojiwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) akizungumzia kuhusu mgogoro wa kisiasa nchini humo, alisema wao walikuwa wamemzoea(Robert Mugabe) kwa hali hiyo hawakuwa na uhakika atakayefuatia utawala wake utakuwaje.Wengine waliohojiwa walisema walikuwa wanapenda mgogoro huo umalizike kwa amani wakitaka kiongozi huyo apewe heshima zake za kuikomboa Zimbabwe hadi kuwa huru hapo mnamo mwaka 1980.

Wapo waliouchukulia mgogoro wa utawala wa Zimbabwe kuwa umekuwa fundisho kwa viongozi wengine barani Afrika wasipende kukaa madarakani kwa muda mrefu. Waliwataja marais wa Uganda,Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwamba ni wakati muafaka kwao kujifunza kutokana na kile kilichotokea nchini Zimbabwe, na  wakubali kuondoka madarakani mapema.

Nchini Uganda, Rais Yoweri Kaguta Museveni kipindi chake cha kuwa Rais kimefikia ukomo, lakini amekuwa akishinikiza kupitia kwa wabunge ili muda wake uongezwe. Naye Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo amekuwa akikwepa kufanyika kwa uchaguzi. Hali hiyo inaendelea kusababisha maandamano ya wananchi wanaotaka uchaguzi huo ufanyike na apatikane kiongozi mwingine. Rais Paul Kagame wa Rwanda, naye vile vile amekuwa akishawishi mabadiliko ya katiba yanayomhalalisha yeye kuendelea kutawala.


Hakuna shaka kwamba Rais Robert Mugabe ataondoka madarakani kwa kuwa wazimbwe wanamtaka afanye hivyo, lakini haitakuwa vyema kama wazimbabwe hao watayasahau yale mema yote aliyoifanyia nchi yake.Inawezekana pamoja na mageuzi ya uongozi ya kupata kiongozi mwingine, siyo kwamba maisha ya Wazimbwe yatakuwa bora zaidi. Yawezekana yakawa mabaya zaidi kuliko hata wakati wa utawala wa Rais Robert Mugabe. Kama alivyozungumza mwananchi mmoja huko huko Zimbabwe, walikuwa wamemzoea Robert Mugabe hawajui ajaye, atakuwaje. Dunia yote inasubiri, lakini historia ya Wazimbabwe haiwezi kumsahau Robert Mugabe.Afrika itamkumbuka kwa kuwa kiongozi jasiri aliyekataa kuburuzwa na mataifa ya Ulaya yanayowataka viongozi wa kiafrika kufanya watakavyo.