Monday, January 08, 2018

CHAMA CHA MAPINDUZI NI TAJIRI KINAJIPANGA KUJITEGEMEA




Yatakuwa ni maumivu makubwa kwa wanachama wabadhirifu wa Chama cha Mapinduzi kwa kulia na kusaga meno. Kamwe haitavumilika mali za chama kufujwa, kuporwa ama kuhujumiwa na wajanja wachache. Hivyo ndivyo sasa Mwenyekiti wa chama hicho Dk. John Pombe Magufuli alivyoanza katika mkakati wake  madhubuti wa kutaka mali za Chama cha Mapinduzi  zote zihakikiwe.

Uhakiki wa mali zote za Chama cha Mapinduzi unalenga kutaka kujua ziko wapi na ni nani anazimiliki, na je kinachopatikana kinafikishwa kwenye chama? Wale waliokuwepo miaka ya sabini na themanini wanaikumbuka baadhi ya miradi iliyokuwa imeshamiri. Kwa kutaja michache, pale Mnazi mmoja jijini Dar es Salaam kulikuwa na duka kubwa la bidhaa mbalimbali. Haikufahamika ni katika mazingira gani duka hilo halikuweza kuendelea..Kuna majengo mengi yaliyopangishwa ambayo inadaiwa yanawanufaisha wajanja wachache. Kwa ujumla Chama cha Mapinduzi kimekuwa na rasilimali nyingi ambazo zimekuwa zikilalamikiwa kuporwa na kusababisha kishindwe kujiendesha na kutegemea kusaidiwa na serikali.

Kwa wanachama wa Chama cha Mapinduzi wanaokitumikia kwa haki bila kutafuta kujitajirisha, wataupongeza msimamo huo wa Mwenyekiti wao ambao ni wa  kukijengea heshima kubwa. Kwamba wanachama wachache ambao walikabidhiwa dhamana ya kusimamia mali za chama hawakujali kuzitunza. Ni hali ambayo ilisababisha kujenga matabaka miongoni mwa wanachama.Isingekuwa rahisi kwa chama kuwa na lugha moja katika kuwaongoza wanachama wake.

Ni dhahiri uhakiki huo wa mali za chama, hautotofautiana sana na uhakiki wa watumishi uliofanyika katika taasisi za serikali. Ulilenga kujiridhisha kuhusiana na idadi yao pamoja na uhakika wa elimu zao kama zilipatikana kupitia mfumo rasmi unaotambulika serikalini.Matokeo ya uhakiki huo yaliweza kubaini kasoro mbalimbali.

Waligundulika watumishi wengi ambao walighushi viwango vya elimu.Ilibainika kulikuwa na watumishi waliokufa na watoro waliokuwa wakiendelea kulipwa mishahara.Kasoro hizo zilikuwa zikiigharimu serikali kulipa fedha nyingi na kuisababishia hasara kubwa.

Chama cha Mapinduzi ni tajiri. Hiyo ni kauli ya Mwenyekiti wake Dk. John Pombe Magufuli aliyoitoa kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama. Anasema dhamira yake kubwa ni kuhakikisha kinajiendesha katika shughuli  zake badala ya kutegemea misaada kutoka serikalini ama wafadhili wengine.

Kuna hatari kubwa kwa chama kama kitategemea misaada kutoka kwa wafadhili. Wanaweza wakawa watu binafsi ama mataifa fulani. Kama ni mtu binafsi amekisaidia chama, ni rahisi kukilazimisha chama kifanye kulingana na matakwa yake. Hali kadhalika kama ni mataifa mengine, yanaweza yakakilazimisha chama kitekeleze itikadi zake tofauti na zile za chama chenyewe.

Tumekuwa tukisikia utegemezi wa chama kutoka kwa wafadhili wakithubutu hata kumchagua mgombea wamtakaye. Hali hiyo imekuwa ni hatari kubwa kwa kuwakosesha wanachama kuwa na nguvu katika chama chao.

Hata wale wanaomsikia Mwenyekiti Dk. John Pombe Magufuli katika hotuba zake, anajisifu kwamba yeye hakufadhiliwa na mtu yeyote.Hakufanya hivyo wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Na ujasiri wake wa kuiongoza serikali na Chama cha Mapinduzi, anabainisha unatokana na yeye kujisimamia na kukubalika kwa wanachama wake bila ya kutumia ushawishi mwingine.

Wale wote waliofuja ama kuficha mali za chama kwa kujisahau, wakati umefika kuzisalimisha ama wao kuwajibika.Wapo watakaolazimika kuadhibiwa wakithibitika kuhusika na makosa hayo.Yote hayo yanafanyika kwa lengo la kukisafisha chama hicho.

Ni mageuzi ya kishindo yanayofuatiliwa na wengi kutoka ndani na nje ya nchi. Ndiyo hayo yanayowakurupusha kutoka upinzani na hatimaye  kujiunga na Chama cha Mapinduzi. Haiwezekani utitiri wa wanachama ukarejea Chama cha Mapinduzi, kama hakuna kazi nzuri inayofanyika.

Ni vyema kabisa kwa wanachama wa Chama cha Mapinduzi wakayaunga mkono kwani yana tija kwa chama chao.Japokuwa baadhi watakuwa wanaumia, hivyo ndivyo ilivyo katika harakati zozote za kuleta mageuzi ya chama.

Maelekezo ya Dk. John Pombe Magufuli kwa kamati aliyoiunda katika uhakiki wa mali za chama, utawahusu hata wanachama walioko serikalini ambao watahojiwa kuhusiana na mali za Chama cha Mapinduzi.

Matokeo ya awali ya mageuzi hayo ni ongezeko la wanachama. Lakini vile vile yapo matumaini makubwa yatakayofuatia ambayo kila mwanachama atayafurahia. Chama kitakuwa na uwezo mkubwa wa kujiendesha bila ya kutegemea ama kuombaomba misaada kutoka mahali popote.

Kuna uhusiano wa waziwazi wa dhamira ya  Dk. John Pombe Magufuli kusafisha uozo wote serikalini na ndani ya Chama cha Mapinduzi .Hali kadhalika siyo rahisi kukiacha chama cha Mapinduzi kikibaki na genge la wezi,wafujaji na mafisadi. Serikali iliyoko madarakani inatekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Ingekuwa siyo haki na wala kutoa taswira sahihi  kama usafishaji wa uozo huo ukabakia serikalini peke yake. Chama cha Mapinduzi kwa nafasi yake ya kuwa madarakani kwa muda mrefu, kinastahili kuonesha mfano wa kuzingatia maadili ya kutotiliwa mashaka.

Siyo muda mrefu wanachama wa Chama cha Mapinduzi watakwenda kwa wanachama ifikapo mwaka 2020, kwenda kuomba kura na kuwanadi  wagombea wao. Sifa pekee itakayowavutia wapiga kura ni kuyatangaza mageuzi hayo yatakayokuwa yamefanyika na kuwanufaisha.

Kwa mfano kuna matukio ya dhati kabisa ambayo wanachama wa Chama cha Mapinduzi wameyashuhudia. Katika uchaguzi wa viongozi wa Umoja wa vijana wa Chama cha Mapinduzi, ilidhihirika jinsi rushwa ilivyodhibitiwa kikamilifu. Mwenyekiti aliyekuwa anamaliza muda wake wa uongozi aliweza kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za rushwa.

Kwenye jimbo la uchaguzi la Singida Kaskazini, mgombea mmoja wa kiti cha ubunge alikamatwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU) kwa tuhuma za kutoa rushwa kwenye kura za maoni. Alifikishwa mahakamani na yuko nje kwa dhamana. Hizo ni jitihada za makusudi kabisa za kuhakikisha wagombea wote ndani ya Chama cha Mapinduzi hawapatikani kwa kutumia fedha ama ghiliba za aina nyinginezo.

Imani ya wanachama wa Chama cha Mapinduzi kwamba hata asiye na fedha, imeanza kurudi kama ilivyokuwa wakati  wa utawala wa hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Nyerere aliwachukia wanachama waliokuwa wakitumia fedha ili kununua uongozi. Hakusita kuwafukuza wanachama wote waliokuwa wakitumia fedha ili kuingia madarakani.Kwa wakati wake chama kiliheshimika na kutumainiwa. Wanachama wa Chama cha Mapinduzi wanaamini sasa Dk. John Pombe Magufuli atakirudisha Chama cha Mapinduzi kwenye heshima yake.Kitaendelea kuheshimika ndani na nje ya Tanzania.