Friday, December 29, 2017

KUSAMEHE NI AFYA KWAKO,JAMII NA KWA MATAIFA

Image resultKUSAMEHE NI AFYA YAKO KWAKO, JAMII NA KWA MATAIFA
‘samahani’ ama kuomba msamaha’(kusamehewa) ni kukiri,kukubali ama kuomba radhi kwamba kuna tendo lisilofaa lililofanyika na kumfanya binadamu mwingine ajisikie vibaya (kuchukizwa)kuumia, kusumbuka ama kukerwa.
Kwa mfano wa kawaida, imekuwa ikisikika kwa Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO)kuwaomba radhi ama msamaha pale huduma zake zinaposababisha usumbufu,ama uharibifu kwa wateja wake. Ama hata Shirika la Reli (TRL) inapotokea kuwa kuna matatizo yanayosababisha ratiba ya usafiri kubadilika,taarifa ya mabadiliko hayo hutolewa na kisha kufuatiwa na kuwaomba radhi (msamaha) wateja wao. Maneno hayo yanapojumuishwa na neno ‘samahani’ mahali popote hutoa ishara ya kutambua na kutaka kujenga uhusiano mwema kati ya pande mbili zinazoshirikiana katika kufikia malengo yao.
Mathalani, mtu anaweza kutamka maneno ambayo binadamu mwenzake yanaweza kumsababishia kupoteza heshima yake na kudharauliwa. Ukimtakia mwenzako kwamba akili zake ni sawa na Mbwa,itamchukiza na kumkera. Kwa kutambua kuwa amechukizwa ama kukerwa na maneno hayo,mtu muungwana atachukua hatua ya kuomba msamaha kwa yule aliyemtamkia maneno mabaya.Wapo binadamu ambao wakiombwa msamaha wanakubali kwa kutamka maneno kwamba wamemsamehe aliyewafanyia yale yasiyofaa. Lakini wapo wengine wanaodiriki kutamka kwamba ‘wanasamehe’ lakini hawatasahau.
Wapo baadhi ya watu ambao wanaweza kuwaomba msamaha ama radhi wale waliowakosea wakiwa wanaonana ana kwa ana. Wapo wengine ambao hukosa ujasiri na huwatumia ndugu zao kuomba radhi ama msamaha.
Katika vitabu vitakatifu kama vile Biblia, umuhimu wa kusamehe ama kuomba radhi vinasisitizwa katika imani ya wakristu.Katika kitabu hicho kitakatifu, Yesu Kristu alipokuwa akifanya kazi ya kuhubiri aliulizwa ni kwa kiwango gani mkristo anatakiwa amsamehe mwenzake? Yesu Kristo aliwajibu kuwa ni saba mara sabini.Wakristo katika mafundisho ya imani yao wanahimizwa kuwasamehe wale wote wanaowakosea bila ya kikomo.
Kupenda kusamehe ni dawa ya afya mwilini. Kushindwa kusamehe ni kuhifadhi sumu mwilini. Padre John Kulwa kutoka Seminari Kuu ya Kanisa Katoliki  Segerea katika jimbo la Dar es Salaam alisisitiza umuhimu wa kusameheana wakati wa mahubiri yake kwa waumini wa Kigango cha Buyuni jijini Dar es Salaam. Alisema kulikuwa na matukio mengi ya baadhi ya watu ambao wamekuwa wakipata matatizo makubwa ya kiafya, kisha kupelekwa Hospitali na kuuguzwa ambapo baadaye hugundulika kuwa chanzo chake ni kukataa kuwasamehe wenzao. Kwamba wanapoamua kuwasamehe wenzao,matatizo yao yanakoma.
Hapa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi(CCM)chini ya Mwenyekiti wake Dk. John Pombe Magufuli tuliona kikitoa msamaha wa kumrejeshea uanachama Sophia Simba aliyekuwa amefukuzwa.
Sophia Simba aliwahi kuwa waziri kwenye serikali ya awamu ya nne na pia kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa CCM (UWT). Aliwahi kuwa mjumbe wa vikao mbalimbali vya Chama Cha Mapinduzi, kama vile Halmashauri kuu.Naye kama katika makala hii inavyojadili, alitambua kuwa alifanya jambo ambalo halikuendana ama lilikiuka maadili ya chama chake hadi kufikia kufukuzwa uanachama.
Katika kutambua kosa lake, Sophia Simba anakiri na kuomba radhi(msamaha) kwa Mwenyekiti wa Chama chake kwa kumuandikia barua. Yeye mwenyewe anaelezea athari alizozipata kutokana na makosa yake. Anakiri zaidi kuwa maisha yake na mafanikio aliyoyapata yametokana na yeye kuwa mwanachama wa Chama cha Mapinduzi. Nao wajumbe wa Halmashauri kuu ya Chama cha Mapinduzi kilichoketi Ikulu jijini Dar es Salaam walikubali kwa kauli moja kumsamehe Sophia Simba kwa yale yaliyotokea. Sophia Simba anakiri kuwa atakuwa mwanachama mwaminifu na mtiifu kwa viongozi wake. Ni dhahiri msamaha wa aina hiyo unatoa fursa ya kuanza ukurasa mpya wa kukijenga chama kipya.Katika maandalizi ya uchaguzi utakaofanyika hapo mnamo mwaka 2020, nguvu yake inahitajika zaidi katika kukipa ushindi wa kishindo Chama cha Mapinduzi (CCM) dhidi ya vyama vya upinzani.
Msamaha huo kwa wanachama wake unajenga imani kwa wanachama wake kuwa pale wanapokosea wanaweza kusikilizwa na kisha kusamehewa. Msamaha ni afya katika kujenga na kuimarisha uhusiano wa watu lakini vile vile hata katika taasisi kuna umuhimu wa msamaha.
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa madaraka kwa Rais aliye madarakani, kutoa msamaha kwa wafungwa walioko gerezani. Ni wakati wakati wa maadhimisho ya miaka 56 ya Uhuru wa Tanganyika Rais Dk. John Pombe Magufuli alitoa msamaha. Wafungwa zaidi ya 8000,walisamehewa vifungo vya maisha, kunyongwa ama kupunguziwa muda wa kukaa gerezani.
Hata nje ya Tanzania yapo mataifa kadhaa ambayo yamewahi kusikika yakiomba msamaha kutokana na makosa yaliyofanywa na kusababisha madhara kwa watu wengine. Matamshi hayo yamekuwa yakichukuliwa kama ishara ya kujutia yaliyotokea na kutaka kujenga uhusiano mwema na imara.