Friday, December 29, 2017

KOFFI OLOMIDE AWAOMBA RADHI WANAWAKE KWA UDHALILISHAJI

Image result for koffi olomideKOFFI OLOMIDE AWAOMBA RADHI WANAWAKE KWA UDHALILISHAJI
Mwanamuziki maarufu kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Koffi Olomide hivi karibuni ametunga wimbo wa kuwaomba radhi wanawake  wote duniani. Umepewa jina la ‘pardon’. Mwanamuziki huyo anasikika akitaja maneno kwa lugha ya Kiswahili, ‘ninaomba radhi’. Kwa mujibu wa matangazo ya Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) Koffi Olomide anawaomba radhi wanawake kufuatia kitendo cha udhalilishaji alichomfanyia mwanamke mmoja wa wachezaji(wanenguaji) wake alipofanya ziara yake ya kutumbuiza nchini Kenya miaka michache iliyopita. Katika tukio hilo, mwanamuziki Koffi Olomide alimpiga hadharani kwa kumuonea. Alilaaniwa na wengi. Serikali ya Kenya kwa kuchukizwa na udhalilishaji huo,  ilimfukuza na kufuta onesho la muziki lililokuwa limepangwa kufanyika nchini humo.
Nayo serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ilimpa adhabu ya kifungo, hata hivyo Olomide hakuweza kuitumikia adhabu hiyo katika hali ya kutatanisha. Kuzembea kwa utekelezaji wa adhabu hiyo kulitoa picha ya upendeleo dhidi ya mwanamuziki huyo. Hakuna uhakika kama wananchi wengine wa kawaida nchini humo wangeweza kupata upendeleo kama alivyofanyiwa Koffi Olomide. Baadhi ya wanawake waliohojiwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza(BBC) walisema Koffi Olomide hastahili kusamehewa kwani udhalilishaji aliomfanyia mwanamke mwenzao haukubaliki. Walisema mwanamke ni kiumbe cha thamani kubwa kinachostahili kuheshimiwa na kutunzwa na wala siyo kuonewa na kudhalilishwa.
Lakini wanaume nao waliohojiwa nchini humo kuhusiana na wimbo wa msamaha huo, wanasema Koffi Olomide anastahili kusamehewa kwa kuwa ameomba radhi na amekiri na kujutia kosa lake. Ingawaje Koffi Olomide amewaomba radhi wanawake,serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ilifanya kosa kwa kushindwa kumuadhibu wakati serikali za mataifa mengine zilikuwa zimetoa adhabu ama  zilionesha kukera na udhalilishaji huo. Serikali ya Zambia nayo ilifuta maonesho ya mwanamuziki huyo, ikionesha kuchukizwa na kukerwa na udhalilishaji huo.
Wanawake wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wanapoukana msamaha wa Koffi Olomide, wanatafakari kwa kile kilichofanywa na serikali yao. Bado wanayo hofu kubwa kwamba inawezekana Koffi Olomide akarufia kosa kama hilo, siyo ajabu serikali yao ikashindwa kuungana nao katika kutetea heshima na utu wao.
Koffi Olomide ametekeleza wajibu wake wa kuonesha kujutia kitendo kibaya na kiovu alichomfanyia binadamu mwenzake. Ingawaje siyo wanawake wote wanaoukubali msamaha wake, anachotakiwa kufanya ni kuwathibitishia wanawake wote kwamba hatarudia tena kuwanyanyasa wanawake. Wanawake popote walipo ni sawa na Mama yake,dada,shangazi,bibi na mke wake. Hakuna uhalali wowote wa kutumia nguvu kuwanyanyasa. Wanastahili mapenzi na kuthaminiwa utu na heshima zao. Kama wanawake hao wanamuudhi kwenye muziki wake,atumie busara na hekima.