Mahakama ya juu nchini Kenya ilimtangaza Uhuru Kenyata
kuwa Rais nchini humo.
Uamuzi huo unatokana na kesi mbili zilizokuwa zimefunguliwa
kupinga matokeo ya uchaguzi uliofanyika mara mbili, wa kwanza ukiwa uliofanyika
mwezi Agosti mwaka huu. Katika uchaguzi huo uliofanyika mwezi Agosti,
Uhuru Kenyata alitangazwa kuwa mshindi.
Tume huru ya Uchaguzi na Mipaka chini ya
Mwenyekiti(IEBC) Wafula Chebukati alidaiwa kuvuruga uchaguzi huo.
Raila Odinga mpinzani wa Uhuru Kenyata alikuwa na matarajio
makubwa ya kupata haki yake kupitia Mahakama hiyo. Kwa mfano pale Jaji David
Maraga alipobatilisha matokeo ya uchaguzi wa marudio , vyama vya upinzani
vilidhani uchaguzi huo ungeweza kurudiwa tena na kuruhusu kuundwa kwa serikali
ya mpito.Wafuasi wa Raila Odinga hawakufurahishwa na maamuzi hayo ilhali wale
wa Uhuru Kenyata walikuwa wakiyafurahia.
Ngome kubwa ya upinzani ya Raila Odinga bado iko katika mji
wa Kisumu,ambako katika uchaguzi wa hivi karibuni ulisusiwa. Kuna wafuasi wengi
wa Odinga kule Mombasa
na sehemu ya mji wa Nairobi.Wote hao bado wanaendeleza upinzani dhidi ya
utawala wa Uhuru Kenyata.
Wakati ambapo kwa sasa kwa kiasi fulani hali ya kisiasa ni
shwari. Rais mteule Uhuru Kenyata anatarajiwa kuapishwa kuitawala nchi ya Kenya .
Wakati Jaji Mkuu David Maraga alipofuta matokeo ya uchaguzi wa mwezi
Agosti,watu wengi walisifia maamuzi hayo.
Kwa mfano hapa nchini Tanzania
wapinzani waliisifia katiba ya Kenya
inayoruhusu matokeo ya uchaguzi kupingwa mahakamani. Inaeleweka hapa nchini Tanzania
kwamba matokeo ya uchaguzi, hususan wa Rais hayawezi kutenguliwa baada ya
kutangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC)
Kuna athari ambazo ziliweza kujitokeza nchini Kenya kufuatia taratibu za kupinga matokeo ya
uchaguzi wa Rais kupitia Mahakamani, ambazo ni kudidimia kwa shughuli za
kiuchumi.Lakini vile vile ni gharama kubwa za kusimamia na kuendesha uchaguzi
ambazo ni kama vile zinapotea bure. Fedha hizo
zingeweza kutumika katika kuendeleza shughuli za maendeleo.
Nchini Tanzania
katiba tuliyonayo ambayo inaipa Tume ya Taifa ya Uchaguzi( NEC) kuwa ndiyo
yenye madaraka ya kutangaza matokeo ya uchaguzi wa kiti cha urais, imesaidia
kukabiliana na madhara yatokanayo na utaratibu wa kupinga matokeo kupitia
Mahakamani. Kitu chema kilichozingatiwa kwenye
Katiba ya Tanzania
, ni kupunguza gharama za kurudia uchaguzi. Katika hukumu iliyotolewa nchini
Kenya na kisha kumtangaza Uhuru Kenyata kuwa Rais, utagundua ni sawa na kile
kilichofanywa na Tume huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC)kwamba ingawaje
ililaumiwa kwa kuvuruga uchaguzi huo, ni kama vile Mahakama ya juu imekubaliana
nayo. Kwa tafsiri nyingine inaweza kuelezwa kwamba Mahakama hiyo ilikuwa
inajaribu kuwapa matumaini wapinzani, kumbe sivyo.
Tulielezwa kuwa wakati Jaji Mkuu David Maraga alipofuta
matokeo ya uchaguzi wa mwezi Agosti, jaji mmoja miongoni mwa waliosikiliza
rufaa ya wapinzani alitofautiana na wenzake. Jaji huyo hakukubaliana na sababu
za kutengua matokeo ya kura za uchaguzi uliompa ushindi Uhuru Kenyata. Sasa
kama wakati ule Mahakama hiyo ilipinga, iweje wapinzani hoja zao
hazikusikilizwa?
Baadhi ya mapendekezo ya wapinzani kuwa ingeundwa serikali
ya mseto inayounganisha pande zote, ama kurudia uchaguzi huo hayakuzingatiwa na
Mahakama hiyo.Huku watu wengi wakiwa
wamejeruhiwa na kuuawa nchini Kenya ,
wananchi wanaendelea kutoridhishwa na ushindi wa serikali iliyoko madarakani.
Kwa kuzingatia kile kilichojitokeza nchini Kenya, kwa
watanzania inabidi tukubaliane kuwa hata kama haki ya wapiga kura inaweza
kupatikana Mahakamani ni maamuzi magumu sana kufuta na kuruhusu uchaguzi
urudiwe.Kwa hekima ya hali ya juu kabisa, kuiachia Tume ya Taifa ya Uchaguzi
(NEC) nchini Tanzania kuwa ndiyo yenye madaraka ya mwisho kuhusiana na
uchaguzi, ni suluhisho la kuepusha migogoro,kupoteza muda wa wapiga kura na
gharama za uchaguzi.
Kwa kadri ya matakwa ya vyama vya upinzani na wanaharakati
wengineo, kutaka kuwe na Tume huru ya uchaguzi kuliko iliyopo kwa sasa ni
sahihi kimaandishi.Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaweza
ikajumuisha kifungu kinachoruhusu wagombea kupinga matokeo ya urais Mahakamani,
lakini kwa uzoefu haitakuwa rahisi maamuzi ya Mahakama kutofautiana na matokeo
yaliyotangazwa na kuthibitishwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC)
Ni vizuri wanaharakati na viongozi wa vyama vya upinzani
wakajikumbusha kwamba hata pale Jaji David Maraga alipotoa hukumu hiyo, walio
wengi walitoa maoni yao wakisema ilikuwa ni ya
aina yake na nadra sana .
Siyo kwamba majaji wa mataifa mengine hawakuweza kutoa hukumu kama hiyo, bali
kwa upande mwingine wanazingatia athari za kiuchumi na za uchaguzi kwa mataifa yao .
Kwa hapa Tanzania
kwa mazingira yetu, bado Tume ya Taifa ya Uchaguzi(NEC) inafaa kuthibitisha na
kutangaza kura za viongozi bora wanaokubalika kwa watanzania na hata wale wa
mataifa ya nje. Ingekuwa kwamba Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ya Tanzania
inawapitisha marais ambao ni hatari kwa usalama na mshikamano wa watanzania,
Tume ya Taifa ya Uchaguzi( NEC) ingekuwa ni muhimu isiwe na madaraka iliyonayo.
Na kwa vyovyote iwavyo, hata kama
wapiga kura watapewa haki ya kwenda Mahakamani ama Tume ya Taifa(NEC) kuwa na
madaraka, haitawezekana maamuzi yake yakawafurahisha wote kwa wakati
mmoja.Watanzania wayakubali matokeo ya uchaguzi kwa kuwa baada ya miaka mitano,maamuzi
mengine yanaweza kufanyika.
Imekuwa siyo ajabu kwa mfano hapa Tanzania , kesi za kupinga matokeo
ya uchaguzi wa wabunge zimekuwa zikichukua muda mrefu kufikia hata zaidi ya miaka miwili. Kwa ulinganifu
huo, kipi kinachofaa kama siyo kusubiri hadi
ifike miaka mitano na kuchagua mbunge mwingine anayekubalika? Watanzania waikubali na waiamini Tume ya Taifa ya
Uchaguzi (NEC)