Monday, January 08, 2018

' FEDHA NYINGI ZA KAKOBE' ZINAWANUFAISHAJE WATANZANIA?





Inawezekana ikawa ni fahari kubwa kwa kiongozi wa dini, Zacharia Kakobe kutamka kuwa ana fedha nyingi kuishinda serikali ya Tanzania.  Kakobe anaweza kujidai ama kuwa na ufahari huo kwa kuziona fedha hizo zikiwa zimerundikana kwenye mifuko ya rambo ama zimetulia Benki. Ni nyingi kwa kadri ya uelewa wake. Hazina faida yoyote  kwa watanzania bali zimewekwa kama mapambo.

Matamshi ya Kakobe kuhusiana na kuwa na  fedha nyingi, yana faida gani kwa watanzania na serikali iliyoko madarakani?. Je,ni kejeli, ni demokrasia ama ni ukosefu wa subira na hekima? Kuwa na fedha nyingi huku wengine hawanazo, kunaleta faraja gani katika jamii?

Fedha za serikali siyo nyingi na wala hakuna ulazima wa kuzitaja kuwa ni nyingi. Fedha za serikali hazipimwi kwa wingi. Fedha za serikali zinapimwa kwa uwezo wake wa kuhudumia wananchi wake. Fedha za serikali kamwe haziwezi kuwekwa zikatulia zikifanywa kama mapambo, bali hugawanywa ili zitanzue matatizo ya wananchi wake.

Mojawapo ya sifa ya fedha za serikali ni kuona wananchi wanavyonufaika nazo. Katika awamu ya tano ya serikali iliyoko madarakani, imedhamiria kutoa elimu bure kuanzia shule ya msingi hadi sekondari. Thamani ya fedha za serikali ndivyo hivyo zinavyoweza kupimwa. Dalili za kufanikiwa kwa mpango huo tayari zimeonekana. Idadi ya wanafunzi wanaojiandikisha kujiunga na shule ya msingi, imeongezeka maradufu. Wazazi wanafurahia maamuzi hayo kwani yamewaondolea kero za michango iliyokuwa ikiwanufaisha wajanja wachache.

Thamani nyingine ya fedha za serikali ni ulinzi wa wananchi pamoja na mali zao.Imeshuhudiwa wakati wa sherehe za Krismas na mwaka mpya wa 2018, Jeshi la Polisi lilivyosimamia kuhakikisha kunakuwepo amani na utulivu. Jeshi la Polisi, liliahidi kuimarisha ulinzi kwenye nyumba zote za ibada wakati wa sherehe hizo. Hata mchungaji Kakobe asingeweza kutoa mahubiri yake kwenye kanisa lake, kama hali ya amani na utulivu ingekuwa siyo ya kuridhisha.

Thamani nyingine ya matokeo ya fedha za serikali, ni pongezi kutoka kwa wananchi wanaponufaika na huduma zitolewazo na serikali. Mathalani, baada ya kumalizika kwa sherehe za Krismas na mwaka mpya 2018, wananchi waliipongeza serikali kwa kuimarisha ulinzi. Wananchi hao walikiri kwamba hapakuwa na matukio ya uhalifu kwenye maeneo yao na kwamba walisherehekea kwa amani.

Siyo jambo jepesi wala rahisi wanapojitokeza wananchi kulipongeza jeshi la polisi kwa kusimamia amani, hususan katika mikoa yote isiyopungua 26 ya Tanzania bara. Serikali inafanya hivyo kwa kuwa inawathamini wananchi wake na isingependa kuona ama kusikia uhuru na haki zao vinahatarishwa na watu wenye nia mbaya.

Ilishuhudiwa katika kipindi hicho, ukaguzi wa magari ya abiria ukifanyika kuhakikisha abiria wanasafirishwa na magari yaliyo imara. Hizo zote ni gharama kwa serikali kwa kutumia rasilimali zake za muda na wataalamu katika kulinda maisha ya wananchi wake.

Wakati wa majanga mbalimbali, tunaiona serikali ikijitokeza kwa kuonesha thamani ya fedha zake kwao. Mathalani katika ajali iliyotokea mkoani Arusha mwaka jana na kusababisha vifo vya wanafunzi, serikali iliweza kugharimia mazishi na kutoa mkono wa pole kwa familia za wafiwa.

Mkoani Kigoma serikali iliweza kufanya hivyo hivyo. Wanafunzi waliokuwa darasani na mwalimu wao, walipigwa na radi na kufariki hapo hapo. Yamekuwa yakitokea matukio ya majanga ya mafuriko ya maji.Baadhi ya watu wamekuwa wakifariki ama kupoteza makazi yao ya awali. Serikali imekuwa ikifanya jitihada kubwa za kuokoa maisha yao.

Katika historia ya kuokoa maisha ya raia wake wa  mkoa wa Dar es Salaam, serikali iliamua kuwagawia wananchi eneo la Mabwepande. Wananchi hao ni wale ambao walikuwa wanaishi eneo la Jangwani,ambako ni bondeni na watu wengi wamekuwa wakisombwa na maji. Hata hivyo baadhi ya wananchi wamekuwa wakikaidi maelekezo ya serikali yanayolenga kuokoa maisha yao.

Hapa jijini Dar es Salaam kuna mradi wa mabasi yaendayo kwa mwendo wa kasi. Mataifa mbalimbali yamekuwa yakifanya ziara za kikazi kuja nchini kujifunza serikali inavyouendesha. Mradi huo wa mabasi unalenga kupunguza msongamano wa magari na kuwawezesha wananchi kufika haraka kwenye shughuli zao za ujenzi wa taifa. Hizo ni jitihada za dhati kabisa zinazothibitisha thamani ya fedha za serikali kwa wananchi wake.

Tunazisikia jitihada za serikali katika kuwekeza kwenye sekta ya afya. Serikali imedhamiria kupunguza idadi ya wagonjwa wanaokwenda kutibiwa nje ya nchi.Wagonjwa watakaokwenda kutibiwa nje ya nchi ni wale tu, watakaothibitika wameshindwa kutibiwa na madaktari wa hapa nchini. Taasisi ya kutibu magonjwa ya moyo ya Jakaya Kikwete ni mojawapo ya viashiria vya mafanikio katika sekta ya afya.

Madaktari bingwa wa taasisi hiyo kwa kushirikiana na madaktari kutoka mataifa mengine   wamethibitisha weledi wao mkubwa kwa kuweza kutibu magonjwa ya moyo, figo na mengineyo ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakipoteza maisha ya watu kwa kiasi kikubwa. Taasisi ya magonjwa ya moyo ya Jakaya Kikwete imeleta ukombozi wa kutibu magonjwa hayo katika ukanda wa  nchi za Afrika Mashariki.

Sambamba na hilo, serikali hivi karibuni ilikifungua chuo cha mafunzo ya tiba, eneo la Mloganzila mkoani Dar es Salaam  ili kuongeza idadi ya madaktari hapa nchini. Yote hayo ni dhamira ya serikali katika kujali afya na uhai wao.

Serikali haioni fahari kuziona fedha zake hazifanyi kazi ya kuwahudumia wananchi wake.Kila kukicha inaingia mikataba na mataifa mbalimbali ili kuhakikisha wananchi wanakuwa na maisha bora.Kuna mradi mkubwa wa umeme utakaojengwa huko Rufiji unaolenga kupunguza tatizo la kukatika kwa umeme.

Kama hilo halitoshi, Reli mpya ya kisasa inakarabatiwa kuanzia Dar es Salaam kuelekea mikoa ya Kigoma na Mwanza.  Abiria watakaokuwa wakisafiri kuelekea mikoa hiyo watakuwa wakitumia wastani wa muda wa saa nane hadi kufika kwao.Licha ya kwamba kutakuwa na unafuu kwa abiria, lakini  uharibifu wa barabara unaosababishwa na magari yanayosafirisha mizigo mizito,utapungua.

Ikiwa mchungaji Zakaria Kakobe atakuwa naye ameyafanya kama hayo yaliyofanywa na serikali, atakuwa amedhihirisha kwamba kweli anazo fedha nyingi zaidi ya serikali.Hakuna mahali ambapo niliwahi kumsikia Kakobe akitajwa ama kupongezwa kwa kuzitumia fedha zake kwa ustawi wa wananchi wa Tanzania. Mathalani, yamekuwa yakijitokeza majanga ya kitaifa kama vile mafuriko ama tetemeko. Sikuwahi kusikia akitoa mchango wake ili kuwanusuru waathirika wa majanga hayo.Sasa madai yake kwamba ana fedha nyingi, yanalisaidia nini taifa letu?

Kuwa na fedha na kisha kuziweka kwenye mifuko ya rambo ili zionekane kuwa nyingi, pasipo kuwaletea ukombozi watanzania hakuna manufaa yoyote bali  hayo ni majigambo tu.

Kuna taasisi nyingi za kidini ambazo zimekuwa zikishirikiana na serikali kuwahudumia wananchi.  Taasisi hizo zimekuwa zikiwekeza kwenye huduma za Afya, Elimu na nyinginezo.

Kitu ambacho mchungaji Kakobe alitakiwa kuwaeleza wananchi ni vipi yeye amewekeza katika sekta mbalimbali ili kutoa huduma kwa wananchi. Kujigamba kuwa yeye ana fedha nyingi zaidi ya serikali hakutakuwa na maana yoyote, kinachotakiwa ni kuwaonesha wananchi kile alichowafanyia kulingana na fedha zake. Na kama amefanya hivyo, kutakuwa na haja ya kulinganisha fedha zake  kama  zitakuwa zinalingana na miradi mingi ya maendeleo iliyotekelezwa  na serikali tangu kupatikana kwa uhuru mnamo mwaka 1961.

Katika majigambo ya Kakobe, serikali yenyewe inaonesha kile inachowafanyia kulingana na bajeti yake.Hata wananchi wenyewe wanakiona na wananufaika.